Alhamisi, 16 Mei 2019

Mpango wa Matumizi Bora ya Ardhi


Shirika  la Hifadhi  za  Taifa Tanzania  (TANAPA) kupitia Idara ya  Ujirani Mwema katika Hifadhi ya Taifa Serengeti linashiriki bega kwa bega katika kutekeleza kazi ya Mpango wa Matumizi Bora ya Ardhi unaoendeshwa na Tume ya Taifa ya Mipango ya Matumizi ya  Ardhi  (NLUPC)  kwa  kushirikiana  na  Halmashauri  za  wilaya  ya  Bunda na Tarime  na  Vi Agroforestry   Tanzania.   Kazi   hii   ambayo   imelenga   zaidi   kutekelezwa   katika   vijiji vinavyopakana  na  Hifadhi  ya  Taifa  Serengeti  (SENAPA)  pamoja  na  Pori  la  Akiba  la Grumenti  (GGR)  ilianza  kutekelezwa  katika  Halmashauri  ya  Wilaya  ya  Bunda  20 Novemba, 2018 hadi 08 Aprili, 2019 na inaendelea katika wilaya ya Tarime. Malengo ya kazi hiyo ni:
v  Kupunguza/ kuondoa migogoro ya matumizi ya ardhi kati ya vijiji jirani na Hifadhi za Taifa Tanzania ambayo imekuwa ikijitokeza mara kwa mara
v  Kutoa Elimu ya Uhifadhi, Usimamizi wa rasilimali ardhi na Sheria zinazohusiana na matumizi ya ardhi nchini hususani sheria namba 5 ya ardhi ya vijiji ya mwaka 1999
v  Kutatua migogoro ya ardhi ikiwemo migogoro ya mipaka na uvamizi wa maeneo ya Hifadhi
v  Kuandaa Mipango ya Matumizi ya Ardhi na kurejea Mipango ya Matumizi Bora ya Ardhi ya vijiji iliyopita muda wake
v  Kumilikisha vipande vya ardhi kwa makundi maalum  ya wananchi wasiojiweza, mathalani wazee, wajane na walemavu
v  Kutoa  mapendekezo  ya  namna  ya  kuboresha  hali  za  maisha  kwa  wananchi kupitia  utekelezaji  wa  miradi  mbalimbali  itakayoibuliwa  wakati  wa  kuandaa mipango ya matumizi ya ardhi ya vijiji.

Uendeshaji Mafunzo na Uhamasishaji
1. Vikao vya Uhamasishaji wa Viongozi ngazi ya Wilaya
Uhamasishaji kwa viongozi wa ngazi ya Wilaya pamoja na Waheshimiwa Madiwani juu ya Uandaaji, Usimamizi na Utekelezaji wa Mipango ya Matumizi Bora ya Ardhi katika vijiji ulifanyika  katika  Halmashauri  zote  mbili  (2)  za  Bunda  Wilaya  na  Bunda  Mji.  Aidha, washiriki wa Uhamasishaji wa zoezi hili walikuwa Mkuu wa Wilaya, Kamati ya ulinzi na usalama,  Wakurugenzi  Watendaji  wa  Halmashauri,  Wakuu  wa  Idara  na  Vitengo  na Waheshimiwa  Madiwani  wa  kata  zinazopakana  na  Hifadhi  ya  Taifa  Serengeti.  Pia uhamasishaji   ulihusisha   Maafisa   Tarafa,   Watendaji   Kata,   Watendaji   wa   vijiji   na Wenyeviti wa vijiji vinavyopakana na SENAPA pamoja na GGR.

2. Mafunzo kwa PLUM za Wilaya
Mafunzo kwa ajili ya Kuzijengea uwezo Mamlaka za Upangaji wa Mipango shirikishi ya Matumizi   ya   Bora   ya   Ardhi   za   Halmashauri   za   Wilaya   (Participatory   Land   Use Management Team -  PLUM) yalifanyika. Timu za PLUM za Halmashauri  ya Wilaya ya Bunda na Halmashauri ya Mji wa Bunda zilijengewa uwezo. Mafunzo yaliyotolewa ni:-
v  Sera, Sheria na miongozo mbalimbali ya uandaaji, usimamizi na utekelezaji wa mipango ya matumzi bora ya ardhi
v  Utayarishaji na Utekelezaji wa Mipango ya Matumizi Bora ya Ardhi
v  Matumizi  ya  picha  za  anga  katika  utayarishaji  na  utekelezaji  wa  mipango  ya matumzi ya ardhi ya vijiji
v   Mafunzo  ya  GIS  na  Land  PKS  (kupima  aina  na  uwezo  wa  ardhi  kwa  kuzalisha mazao).

3 Mafunzo kwa Halmashauri za vijiji (VCs), kamati za VLUM na BLAK
 Tangu zoezi hili kuanza mnamo Novemba 20, 2018 hadi kufikia Aprili 04, 2019 jumla ya vijiji 7 vilipatiwa Mafunzo kwa ajili ya kuvijengea uwezo Halmashuri za Vijiji (Mamlaka za Upangaji) na Kamati ya Usimamizi wa Mipango ya Matumizi ya ardhi ya Vijiji (Village Land Use Management - VLUM) pamoja na Mamlaka za utatuzi wa migogoro ya Ardhi vijijini (Baraza la Ardhi la Kijiji – BLAK) wa kuandaa, kusimamia na kutekeleza mipango ya   matumizi   bora   ya   ardhi   pamoja   na   kutatua   migogoroya   Ardhi   vijijini.   Vijiji vilivyopatiwa  mafunzo  hayo  ni  Hunyari,  Kihumbu,  Mariwanda,  Sarakwa,  Mugeta, Kyandege   na   Tingirima   katika   Halmashauri   Wilaya   ya   Bunda.   Pia   kamati   hizo zimefundishwa sheria mbalimbali za Ardhi ikiwa ni pamoja na:
v  Sera ya Ardhi ya mwaka 1995
v  Sheria ya Ardhi Na 4 ya mwaka 1999
v  Sheria ya Ardhi ya vijiji Na 5 ya mwaka 1999
v  Sheria ya uandaaji wa mipango ya matumizi ya Ardhi Na 6 ya 2007
v  Sheria ya mahakama (utatuzi wa migogoro ya Ardhi) Na 2 ya mwaka 2002
v  Sheria Na. 5 ya Uhifadhi Wanyamapori ya mwaka 2009.

Baadhi ya vijiji ambavyo zoezi hili limefanyika ni;   Hunyari, Kihumbu, Sarakwa, Tingirima, Kyandege,  Mugeta, na Mariwanda katika wilaya ya  Bunda.

Kauli mbiu yetu

BUFADESO kwa maendeleo ya wakulima

MUHIMU

Makala na picha zinazochapishwa katika blogu hii ni kwa ajili ya taarifa na kumbukumbu za Shirika la Bunda Farmers Development Support Organization (BUFADESO)
Hairuhusiwi kutumia yaliyomo katika blogu hii (HASA PICHA) kwa shughuli zozote bila ruhusa ya mmiliki wa blogu hii ambaye ni BUFADESO