Jumanne, 21 Februari 2017

UFUGAJI WA KUKU WA KIENYEJI

Kuku wa kienyeji ni kuku wanaopendwa kufugwa na kuliwa na watu wengi kutokana na uasili wake. Jina la kuku wa kienyeji limekuwa maarufu kutokana na asili(mbegu) ya kuku hawa kutoka katika mazingira yetu tunayoishi, pia mazingira ya ufugaji wake. Ni dhahiri kwa sasa kuku wa kienyeji wamekuwa ghali na wana thamani kubwa kuliko kuku wa kisasa. hii inadhirisha ubora wake na sifa zake kama zinavyoainishwa hapa chini:

A.SIFA ZA KUKU WA KIENYEJI
1. Wanavumilia magonjwa. Kuku wa kienyeji ni wastahimilivu wa magonjwa lakini ni muhimu wakikingwa na magonjwa ya kuku kama mdondo, ndui ya kuku n.k kwa kuwapa chanjo ili kuweza kuwaendeleza.
2. Wana uwezo wa kujitafutia chakula ardhini. Wanao uwezo wa kuchangamka katika mazingira kwa kuparuaparua ili wapate chakula.
3. Wana uwezo wa kuatamia mayai, kutotoa na kulea vifaranga na ustahimilivu wa mazingira magumu kama ukame, baridi n.k
4.Nyama na mayai yake vina ladha nzuri kuliko kuku wa kisasa. Pia virutubisho vilivyomo katika mayai na nyama ya kuku wa kienyeji ni vingi kuliko kuku wa kisasa.
5. Wana uwezo wa kujilinda na maadui kama mwewe n.k . Pamoja na sifa hizi ni muhimu muhimu kuku hao wakapewa matunzo mazuri, wakawekwa kwenye mabanda mazuri, wakapewa maji na chakula cha kutosha.

B.FAIDA ZA KUKU WA KIENYEJI.
-1. Mayai huweza kutumika kwa tiba.  
-2. Kiini cha njano cha yai kinaweza kutumika kutengenezea mafuta ya nywele (shampoo)
-3. Manyoya yake yanaweza kutumika kama mapambo.
-4. Kinyesi cha kuku kinaweza kutumika kama mbolea kwa mazao na pia kama chakula cha samaki.
-5. Nyama ya kuku ni kotoweo kitamu kinachopendwa na kila mtu.
-6. Tangu enzi jogoo amekuwa akitumika kutumbusha muda/wakati hasa wakati wa alfajiri pale anapowika.
-7. Kuku wakifugwa vizuri ni ajira yenye faida kubwa kwa mfugaji.
 

C:MAPUNGUFU
Yako mapungufu mengi yanayofahamika lakini hapa naomba niweke lile la muhimu zaidi. MAGONJWA kama mdondo na ndui huathiri ufugaji wa kuku kutokana na kutokuzingatia kuchanja kuku kwa wakati.


D: KABILA ZA KUKU WA KIENYEJI
Kuna maelezo ya kusisimua sana kuhusu makabila ya kuku wa kienyeji, hata hivyo kuna ugumu kidogo kuweza kuyachanganua makabila hayo kutokana na muingiliano mkubwa wa vizazi kati ya aina mbalimbali za kuku hao. Hata hivyo kuku hawa wana tofauti za kimaumbile zinazosaidia kwa kiasi fulani kutambua uwepo wa baadhi ya makabila ya kuku. Kabila hizi pia zinahusishwa kwa kiasi kikubwa na eneo kuku wanakotoka. Baadhi ya kuku wa kienyeji wanaweza kutambuliwa kwa maumbile yao Mfano:

a.
 Kishingo - kuku wasio na manyoya shingoni
b.
 Njachama au Nungunungu - Hawa ni wale wenye manyoya yaliyosimama.
c.
 Kibwenzi - Ni wale wenye manyoya mengi kichwani.
d.
 Kibutu- Hawa hawana manyoya mkiani
Mwingiliano wa vizazi unaweza ukasababisha kuku kuwa na aina ya maumbile mchanganyiko. Mfano kuku aina ya kuchi anaweza kuwa na alama ya kishingo, Njachama, Kibwenzi au Kibutu.

Hivyo kabila za kuku zifuatazo zinaweza kutambuliwa kama ndiyo kabila za kuku wa kienyeji kulingana na maumbile yao na maeneo wanakotoka.
(i)          KUCHI
Ni kuku warefu kwa umbo na wenye kusimama mgongo ukiwa wima. Wana manyoya machache mwilini na hasa kifuani, vilemba vyao ni vidogo. Majogoo huwa na wastani wa uzito wa Kg. 2.5 na mitetea kg 1.5 mayai ya kuchi yana uzito wa wastani wa gm 45. Kuku hawa hupatikana kwa wingi maeneo ya Mwanza, Shinyanga, Tabora na Zanzibar.

(ii) CHING'WEKWE

Kuku hawa ambao jina lao ni gumu kidogo kwa mtu asiyekuwa na meno kulitamka wana sifa zifuatazo.
Majogoo wana wastani wa kg 1.6, Mitetea wastani kg 1.2, mayai wastani wa gm 37. Kuku hawa wenye umbo dogo hupatikana zaidi maeneo ya CHAKWALE mkoani Morogoro na pia sehemu za umasaini. Kuku hawa hutaga mayai mengi sana kuliko aina nyingine ya kuku wa kienyeji waliopo Tanzania, kwa hiyo wanafaa sana kwa biashara ya mayai.


(iii)UMBO LA KATI

Majogoo wana uzito wa wastani wa kg. 1.9, Mitetea kg. 1.1, Kuku hawa ndio hasa wanaoitwa wa kienyeji(wa kawaida) Wana rangi tofauti. Utafiti umeonyesha kuwa kuku hawa hukua upesi na hupata kinga upesi baada ya kuwachanja dhidi ya ugonjwa wa mdondo (Castle desease)
Muhimu - Mfugaji akifanya uchaguzi kutoka kwenye aina hii ya kuku na kutoa matunzo mazuri kwa hao kuku waliochaguliwa, Hakika anaweza kupata kuku walio bora na wenye uzito wa kutosha pia kutaga mayai mengi na makubwa.


(iv) SINGAMAGAZI

Ni aina ya kuku wakubwa wa kienyeji wanaopatikana zaidi TABORA, kuku hawa wana utambulisho maalum kutokana na rangi zao. Majogoo huwa na rangi ya moto na mitetea huwa na rangi ya nyuki. Uzito - Majogoo uzito wa wastani wa kg 2.9, mitetea wastani wa kilo 2 mayai gramu 56.

(v) MBEYA
Kuku hawa wanapatikana Ileje mkoani mbeya. Asili hasa ya kuku hawa ni kutoka nchi ya jirani ya Malawi na si wa kienyeji asilia bali wana damu ya kuku wa Kizungu "Black Australop". Majogoo Kg 3 mitetea kg 2 mayai gram 49

(vi) PEMBA 
Hupatikana zaidi Pemba. Majogoo Kg.1.5 Mitetea Kg 1 mayai wastani gm 42

(vii) UNGUJA.
Majogoo Kg 1.6, mitetea kg 1.2 mayai gm 42. Kuku hawa wa Unguja na Pemba wanashabihiana sana na Kuchi isipokuwa hawa ni wadogo.
u

KWA UFUGAJI BORA WA KUKU WA KIENYEJI YAPASWA KUZINGATIA YAFUATAYO:
I. Usafi wa vyombo na mazingira ya kuku
Eneo na banda la kufugia kuku wako yapaswa liwekwe safi muda wote kwa kuzingatia yafuatayo:
1.  Vyombo vya chakula na maji visafishwe mara kwa mara kwa maji safi na sabuni.
2.  Pumba au chakula kilicholowana na kuchanganyika na kinyesi cha kuku kitolowe na kufukiwa.
3.  Choma moto au zika kwenye shimo refu kuku waliokufa kwa ugonjwa.
4.  Usifuge kuku na ndege wa jamii nyingine kwa mfano bata katika banda moja.
5.  Ondoa mbolea mara kwa mara kutoka katika banda la kuku.
6.  Tumia dawa za kuulia vimelea kusafishia banda na upake chokaa angalau mara moja kwa mwaka.
7.  Ziba matundu yote yanayoweza kuruhusu panya na wanyama wakali kama vicheche kuingia katika banda la kuku.

II. Wapatie kinga na tiba kuku wako kila mara:
Changamoto kubwa ya ufugaji wa kuku ni kuathiriwa na magonjwa. zingatia na kuwa makini katika kukabiliana na changamoto hii. Magonjwa yanayoshambulia kuku ni pamoja na:
Ndui ya kuku
Huathiri sana vifaranga wanaokua na ujitokeza kwa wingi wakati wa mvua za muda mrefu. Husababisha vivimbe katika uso/ kishungi na hata sehemu nyengine zisizo na manyoya.
Mdondo/kideri
Mdondo, au kwa majina mengine lufuo, au kideri ni ugonjwa hatari katika magonjwa ya kuku wa asili. Ni ugojwa wa virusi ambao huathiri kuku wa rika zote, huweza kuangamiza kuku wote kijijni.
Ukosefu wa vitamini A
Ugonjwa huu husababisha macho kuvimba na kutoa uchafu mziito kama sabuni iliyolowana. Kuku wenye dalili hizi hawaponi na hata kufa. Ugonjwa hujitokeza baada ya kipindi kirefu cha kiangazi kwa ajili ya ukosefu wa majani mabichi.
Kosidiosisi
Huathiri kuku wa umri wowote lakini huuwa zaidi vifaranga na kuku wanaokua. Kuku hudhoofika, manyoya huvurugika na kuku huwa kama wamevaa koti. Kuku huarisha damu au kinyesi cha kahawia na huzubaa na kuonekana kama wamevaa koti.
Viroboto, chawa na utitiri
Hawa ni wadudu wa nje wanaoshambulia ngozi. Huweza kusababisha ugonjwa kutokana na kunyonya damu. Viroboto hushambulia kichwa na kunata huku wakinyonya damu. Viroboto huuwa vifaranga. Chawa na utitiri hughasi kuku hadi wakashindwa kutaga na kuatamia.
Minyoo
Minyoo huweza kudhofisha kuku na kuwafanya waweze kuugua maradhi mengine kirahisi. Muone mtaalaam ukihisi kuku wako wana minyoo.
III. Wape kuku Chakula cha kutosha
1.  Wapatie vifaranga nyongeza ya protini kwa kuwachanganyia vumbi la dagaa au vichwa vya dagaa vilivyotwangwa kwenye pumba za mahindi.
2.  Changanya kikombe kimoja cha vumbi la dagaa na vikombe vitano vya pumba za mahindi (tumia kikombe kidogo cha chai).
3.  Mchwa na wadudu wengine wanaweza kutumika kama nyongeza ya protini.
4.  Vuna mchwa kwenye vichuguu au tengeneza mchwa katika njia za mchwa.
5.  Kutengeneza mchwa: changanya kinyesi cha ng’ombe na majani makavu, mabua ya mahindi au maranda ya mbao katika chungu au ndoo ya zamani.
6.  Mwagia maji hadi kila kilichomo kilowane kisha weka katika chombo kama ndoo au chungu. Weka chombo chako katika njia ya mchwa ukikigeuza juu chini na subiri hadi kesho yake asubuhi, kisha beba vyote vilivyomo na uwamwagie kuku mahali walipo.

IV. Tafuta vifaranga bora
Fanya yafuatayo ili uweze kutotolesha vifaranga bora ambavyo vitakupatia kuku bora na wazuri
Chagua jogoo bora na tetea bora kuzalisha kuku.
Sifa za jogoo bora
1.  Awe na umbo kubwa, awe ukiko mzuri na usioangukia upande mmoja.
2.  Apende kuwa na himaya yake. Ukimpata jogoo mwenye sifa hizi mueke yeye na matetea kumi. Hivyo ukiwa na matetea ishirini jogoo wawili wanatosha.
       Sifa za tetea bora
Tetea bora ni yule mwenye umbo kubwa, mwenye uwezo wa kutaga mayai ya kutosha, kuatamia na hatimaye kutotoa vifaranga.
Uhifadhi wa mayai
1.  Weka mayai mahali safi na penye hewa ya kutosha.
2.  Tumia kasha lililokatwa na kujaza mchanga mkavu na safi au kasha la kuhifadhia mayai.
3.  Weka sehemu butu ya yai iwe upande wa juu na ile iliyochongoka itizame chini.
4.  Andika namba au tarehe katika siku lilipotagwa.
5.  Mayai yakishatagwa yatolewe na kuhifadhiwa na moja liachwe kwenye kiota ili kumuita kuku kuja kutaga kesho yake.
Kuatamiza mayai
1.  Kuku awekewe mayai yatakayokuwa na uwezo wa kuyaatamia na kuyatotoa yote.
2.  Mayi 10 hadi 12 yanatosha kuatamia.
3.  Mayai ya kuatamiza yasizidi wilki 2 toka kutagwa.
4.  Yai la mwisho kutagwa liwe la kwanza kuchaguliwa hadi yapatikane mayai 10 mpaka 12, na apewe kuku wa kuyaatamia.
5.  Mayai ya kuatamiza yasafishwe kwa kitambaa kikavu na safi au kilichowekwa spiriti
Kutotolesha vifaranga wengi kwa wakati mmoja
1.  Kama unataka kuku zaidi ya mmoja watamie na kutotoa kwa mpigo fanya yafuatayo;
2.  Kuku wa kwanza akianza kuatamia muwekee mayai yasiyo na mbegu mfano mayai ya kuku wa kisasa au kuku asiye na jogoo.
3.  Rudia zoezi hilo hadi utakapofikisha kuku watano kisha wawekee kuku wote mayai yenye mbegu.
V. Tunza vizuri vifaranga ili waweze kukua
Vifaranga wengi hufa kabla ya kufikisha miezi miwili kutokana na magonjwa, baridi na kuliwa na wanyama wengine. Ili kupunguza vifo vya vifaranga wa siku 1 hadi miezi miwili zingatia yafuatayo;

Ulinzi dhidi ya mwewe na wanyama wengine
1.  Weka vifaranga kwenye tenga na kuwafunika ili wasiende mbali wakati wa mchana. Wape maji na chakula. Hakikisha hawapigwi jua wala kunyeshewa mvua. Wakati wa usiku walale na mama yao.
Chanjo ya mdondo kideri/lufuo
Kama tetea alichanjwa kabla ya kuanza kutaga vifaranga wanaoanguliwa huwa na kinga ya mdondo ya kuwatosha kwa wiki 3 za kwanza za maisha yao. Wachanje vifaranga hao dhidi ya mdondo wafikishapo umri wa siku 18.
Vifaranga ambao historia ya chanjo ya mama haijulikani, wapewe chanjo ya mdondo siku tatu baada ya kuanguliwa, rudia hadi wakifikisha wiki tatu kisha uchanje kila baada ya miezi 3
Kinga dhidi ya kosidiosisi
Kinga ya kosidiosisi kwa vifaranga, itolewe hata kama ugonjwa haujajitokeza.
1.  Wape dawa ya amprolium kwa muda wa siku tatu mfululizo mara wafikishapo siku saba tokea waanguliwe kama kinga ya kosidiosisi.
2.  Dawa inaweza kutolewa hata kama wamevuka umri huo. Fuata maelekezo ya mtaalam juu ya kiasi cha dawa kinachopaswa kuchanganwa katika maji au pumba
3.  Kama vifaranga wadogo wataonesha dalili za kuzubaa kama kuvaa koti wapewe dawa ya amprolium kwenye maji kwa utaratibu ufuatao;
Dawa siku tatu mfululizo: usiwape kwa siku mbili; gawa tena kwa siku tatu

MAMBO YA JUMLA YA KUZINGATIA
1.  Hakikisha banda na vyombo vya chakula cha kuku ni visafi kuepusha magonjwa.
2.  Usichanganye kuku na bata katika banda moja. 
3.  Lisha chakula cha ziada hasa kwa vifaranga.Unaweza kununua chakula maalum au kujitengenezea mwenyewe.
4.  Kideri, kosidiosisi, ndui na upungufu wa vitamini A ni vyanzo vikuu vya vifo vya kuku wako. Kumbuka kukinga kuku wako dhidi ya magojwa haya.
5.  Kumbuka kuchagua mayai ya kuatamiza kama ilivyoelekezwa ili kuepuka kupata mayai viza.
6.  Vifaranga wadogo hadi wiki nane huhitaji matunzo mazuri, fuata maelezo kuzuia vifo.Kumbuka unapopoteza kifaranga ni hasara kama unavyopoteza kuku mzima tetea/jogoo.
7.  Kumbuka ukiuza kuku wengi kwa mpigo utaongeza mapato yako, jitahidi kuzalisha vifaranga kwa wingi ili upate kuku wengi baadae.
8.  Muone mtaalam wa mifugo ulie karibu nae kwa ushauri zaidi.
9.  Soma maelezo haya mara kwa mara na ufanye yalioelekezwa.
10. Washirikishe wengine katika kaya yako ili nao wajifunze na kufanya hivyo kukuza ufugaji na kipato cha familia.Katika kaya nyingi kuku ni mifugo ya watoto au kinamama. Familia ilishiriki kwa pamoja na kwa usawa, kuku watapata huduma na mahitaji yao na mwisho wa siku faida itanufaisha familia nzima. 

Jumamosi, 4 Februari 2017

Meneja wa Vi Tanzania Bi Gudrun Bostrom (wa pili kushoto aliyekaa) na Afisa Uhakiki Viwango Bi Flora Josephat (aliyekaa mwanzo kushoto) wakiwa katika picha ya pamoja na Bodi ya Wakurugenzi wa shirika la BUFADESO

Jumatano, 25 Januari 2017

JINSI YA KUANDAA MPANGO MKAKATI

NINI MAANA YA MPANGO:
·         Ni mlolongo wa mawazo, shughuli, michakato au matendo; ulioandaliwa kwa wakati uliopo ili uweze kutekelezwa au kufanyiwa kazi wakati ujao.
·         Kwa kifupi ni matarajio na matazamio ya mambo/shughuli za kufanya baadae.
·         Shirika linaweza kuwa na mipango tofauti kama vile mpango kazi, mipango ya bajeti, mipango ya uongozi na utawala, mpango mkakati n.k

Kupanga ni nini?
1.      Kupanga ni kuchagua.
2.      Kupanga ni kuchukua picha ya yaliopita, kulinganisha na hali ya sasa ili kuleta matokeo bora.
3.      Kupanga ni mchakato wa kueleza na kuelewana miongoni mwa watu wanaofanya kazi pamoja ili kuleta mabadiliko fulani.
4.      Kuweka msingi wa maamuzi kwa ajili ya utekelezaji wa shughuli za miradi. 

KWA NINI TUNAHITAJI KUPANGA?
Ø  Ili kupanga rasilimali za mradi na kufikia matokeo bora iwezakanavyo ili kufikia malengo.
Ø  Kujua rasilimali zinazotakiwa, muda, uhalisia n.k.
Ø  Kuweka malengo kwa shughuli za mradi.
Ø  Kuamua viashiria vya ufuatiliaji na tathimini na muundo wa utoaji taarifa.
Ø  Kuratibu na kushirikiana na wengine ili kuepuka upotevu wa muda, vifaa, fedha, nguvu, nishati n.k.
Ø  Kuhakikisha mfuatano bora wa utekelezaji wa shughuli ili kuepuka matatizo yasiyo ya lazima.
Ø  Kupata mwongozo wa bajeti.
Ø  Kufanya maandalizi kabla ya utekelezaji ili kufahamu shughuli tunazowajibika kuzitekeleza.

v  Kwa kuwa mambo haya yanalenga kupata matokeo bora, bila shaka kunahitajika zana bora.
v  Kwa mtu yeyote anayetarajia kufanya shughuli yoyote, lazima ahakikishe kuwa nyenzo zake za kazi ni bora. Mfano Mkulima anahitaji jembe bora.
               Mchoraji anahitaji brush bora.
v  Zana ya shirka katika kupanga ni DIRA.



MAANA YA MKAKATI:
n  Mkakati kwa maneno rahisi ni mpangilio katika mtiririko wa maamuzi. Hujumuisha mambo  yanayolenga kufikia hali endelevu katika ushindani. Mkakati  unahusiana  na shauku ya kuwa tofauti kwa kuleta matokeo chanya.

MAANA YA MPANGO MKAKATI
·         Ni mchakato maalumu unaolenga kutambua na kufanyia kazi mambo/shughuli/changamoto anuai kwa njia shirikishi ili kufikia matokeo yanayolengwa.
·         Mpango Mkakati ni mpango wa jumla wa maendeleo ya taasisi husika unaopangwa kwa kuzingatia mambo yafuatayo:
ü  Changamoto zinazoikabili taasisi husika katika mazingira ya ushindani
ü  Hali halisi ya mazingira ambamo taasisi hiyo imo
ü  Uwezo wa taasisi husika katika kutekeleza majukumu yake
ü  Dira, dhamira na malengo ambayo taasisi imejiwekea
ü  Sera na sheria za nchi zinazotawala shughuli za taasisi husika
·         Mpango mkakati unahusisha mchakato wa kuchanganua hali ya ushindani wa taasisi, kutayarisha dira, dhamira na malengo ya taasisi, kuandaa mpango wa utekelezaji na kutafuta rasilimali zitakazosaidia kufikia malengo yaliyowekwa.
·         Ili mpango uwe mpango mkakati ni LAZIMA:         
                                                -Uonyeshe muelekeo wa wapi tunalenga kufika.
                                                -Uwe na muda maalumu wa kufikia matarajio.
                                                -Kuwe na malengo ya muda mfupi na muda mrefu.
                                                -Kuwe na vipaumbele vya miaka mf miaka 3, 5 au 10

FAIDA ZA KUWA NA MPANGO MKAKATI KATIKA SHIRIKA
        i. Unapunguza uwepo wa ushindani na kurahisisha fursa ubia na mashirika/taasisi nyingine.
      ii. Unatoa picha ya wazi ya nini shirika linafanya.
    iii. Unasaidia kutambua na kufikia dira, dhamira na malengo ya shirika.
    iv. Unaleta dhana ya Umiliki.
      v. Unachochea uwajibikaji kwa matokeo mazuri.
    vi. Unahamasisha wafadhili na mashirika mengine kusaidia shirika.
  vii. Unaainisha uwazi wa utendaji kazi kwa washiriki.
viii. Unarahisisha tathmini ya muda na shughuli.
    ix. Unaainisha walengwa wa shughuli.
      x.Huunda mazingira ya kufanya maamuzi.




KWA NINI SHIRIKA LINAHITAJI MPANGO MKAKATI?
(a)    Mpango mkakati Unasaidia shirika kuwa na utawala/uongozi bora.
(b)   Unawezesha shirika kuweza kutofautishwa na mashirika/taasisi nyingine zinazofanya kazi zenye kufanana na shirika letu.
(c)    Unasaidia shirika/taasisi kutengeneza sera.
(d)   Mpango mkakati unasaidia shirika/taasisi kuaminika  na kupewa mtazamo mzuri
(e)    Unasaidia shirika kuwa na umakini na uwazi katika utendaji wa shughuli zake.
(f)     Unasaidia shirika kuwajibikia/kufanya maamuzi kabla ya matokeo na si baada ya matokeo  (proactive rather than reactive)


NI MUDA GANI SHIRIKA LINATAKIWA KUANDAA MPANGO MKAKATI
1)      Pale shirika linapoanzishwa.
2)      Pale dira, dhamira na vipaumbele vya shirika vitakapobadirishwa.
3)      Pale sababu za nje zinapoathiri na kuleta mgongano katika shirika.
4)      Pale shirika linapohitaji kuongeza malengo yake.

TAARIFA/NYARAKA ZINAZOHITAJIKA WAKATI WA KUANDAA MPANGO MKAKATI:
             I.            Katiba ya shirika.
          II.            Muundo wa shirika.
       III.            Ripoti za shirika.
       IV.            Sera za serikali
          V.            Mpango mkakati wa nyuma
       VI.            Ripoti za tathmini ya mahitaji
    VII.            Upembuzi yakinifu/utafiti wa majaribio
 VIII.            Malengo na shughuli za shirika.
       IX.            Mpango mkakati wa shirika mama au shirika rika.


MCHAKATO WA KUTAYARISHA MPANGO MKAKATI
·         Mchakato wa kutayarisha mpango mkakati kwa kawaida hufuata hatua kuu nne muhimu kama ifuatavyo:

(a)    Uchambuzi wa hali halisi
·         Ni ipi hali halisi ya taasisi kwa sasa?
·         Hatua hii inahusisha uchambuzi wa taasisi yenyewe na mazingira yanayoizunguka
·         Lengo la kuichambua taasisi husika ni kufahamu uwezo (strengths) na udhaifu (weaknesses) wake. Uchambuzi huu hufanywa kwa kuangalia dira, dhamira na malengo ya taasisi husika.
·         Lengo la kutathmini mazingira yanayoizunguka taasisi ni kutaka kupata ufahamu wa fursa (opportunities) na vikwazo (threats) vya taasisi husika.

Kazi ya wana Bodi: Chambua hali halisi ya shirika letu la BUFADESO



(b)    Uandaaji wa mpango mkakati
·         Taasisi inataka kuwa ya namna gani?
·         Kutayarisha dira, dhamira na malengo ya taasisi
·         Kuandaa mpango wa maendeleo ambao unaonyesha malengo, matendo/shughuli, muda wa utekelezaji, wahusika, rasilimali na viashiria vya ufanisi
           
 Kazi: Fafanua dira na dhamira ya shirika letu
           
(c)    Utekelezaji wa mpango
·         Taasisi itafikaje kule inakotaka kufika?
·         Wakati wa utekelezaji wa mpango sharti taasisi izingatie muundo wake wa utendaji, kugawa rasilimali kwa kufuata vipaumbele, kuhakikisha kuwa watumishi waliopo wanatosha na wana ujuzi unaotakiwa.
·         Mpango wa utekelezaji wa mwaka pamoja na bajeti huandaliwa kwa kuzingatia uwezo wa taasisi husika
·         Baada ya fedha za utekelezaji kupatikana mpango kazi huandaliwa ukiwa ni mwongozo wa utekelezaji

Kazi: Chora muundo wa shirika letu

(d)   Ufuatiliaji na tathmini ya mpango
·         Taasisi itajuaje kwamba imefika mahali ilipokusudia?
·         Ufuatiliaji hufanywa ili kufahamu ni kwa kiasi gani taasisi imefikia malengo yake kwa kuzingatia dira na dhamira.
·         Kwa kufanya ufuatiliaji na tathmini taasisi huweza kuchukua hatua za marekebisho pale ambapo mambo hayajaenda vizuri. Iwapo mpango kazi hautekelezeki vizuri, Yapaswa malengo, shughuli au mikakati inayotumika haijawekwa vizuri, au haitekelezeki na hivyo marekebisho yaweza kufanywa kwenye lengo au mikakati inayotumika.

            Swali: Ni zana ipi inatumika katika ufuatiliaji na tathmini katika shirika lenu

MUUNDO WA MPANGO MKAKATI
1.      UTANGULIZI:
Katika kipengele hiki, unaweza kuwatambua au kuwashukuru wadau waliowezesha Shirika kwa namna moja au nyingine.
2.      UTAMBULISHO:  
Kutambulisha shirika kwa ufupi kuhusu aina ya Shirika, jinsi lilivyoanzishwa na kusajiliwa,  eneo la kazi na Idadi ya wanachama.
3.      DIRA, DHAMIRA, MAADILI NA WALENGWA
                DIRA
Dira ya Shirika ni ndoto/maono/taswira ya kifikra ya jinsi mafanikio ya mbele yatakavyo kuwa. Dira huelezea ni vipi/nini shirika linahitaji kuona miaka ya mbele. Dira huweka msingi imara katika shughuli mkakati. Huwezesha kufanya uchanganuzi wa mipango mkakati na shughuli. Kwa hali hiyo dira ni sehemu muhimu katika mchakato wa kupanga kimkakati
                             
 UBORA   WA DIRA 
Ukitaka  kuhakikisha  ubora  wa  dira   yako,  jiulize  maswali  yafatayo:
1:  Je, inaelekeza  kile  ninataka  kufikia?
2: Je, inaendana  na  shughuli  ninazo  kusudia  kufanya?
3:  Iko  wazi kiasi  cha    kuvunjwa katika  malengo  kadhaa?
4: Ipo  wazi  kiasi   cha  kuelewaka  kwa  watu,  kushawishi  na   kusisimua?
5: Inaweza  kuandaa  juhudi mioyoni mwa watu   na  kujitoa?

DHAMIRA 
Dhamira ni wito/utume  wa shirika unaojumuisha shirika litafanya vipi {kazi ya muda mrefu} kufikia dira.
Dhamira  hueleza shughuli  na  kiwango  cha  shughuli  zinazotekelezwa  na  shirika  au  taasisi

DHAMIRA YAWEZA KUFANYA  NINI?
Dhamira inaeleza shughuli za shirika inajibu   swali:  
 Kwa nini tuko hapa?
Huelezea  kiwango.  Nani tunamhudumia na kwa namna   gani? 
Huonesha  mwelekeo  na   mkakati  mkubwa  unaokua  kiongozi   kwa  maamuzi  ya   ngazi  ya chini
Hujibu , tunashirikije  sisi   kama  wanachama  wa  shirika  ili   kuleta  mapinduzi?

KUELEWA    KAMA DHAMIRA NI   SAHIHI
  Tujiulize maswali yafuatayo
-          Inaeleweka?
-          Inafikika?    au ni ya kufikirika? 
-          Inaelezea mambo ambayo shirika linayalenga?
      -     Shirika  linamhudumia    nani?
      -     Inaendana   na       
ü  Dira   yangu binafsi?
ü  Dira ya wadau?
ü  Dira ya shirika?
MAADILI;
Haya   ni matamko   yanayobainisha    falsafa  shirikishi  za  shirika

Matamko  haya  yana   kazi  gani  ?
·         Hutoa  misingi  ,kanuni  na  imani  zinazolinda   menejimenti  ya  shirika  mahusiano  ya  wafanyakazi  na  mahusiano  ya  wadau  na  shirika
·         Hueleza  viwango  muhimu  na  tabia zinazotakiwa  na  shirika
·         Hueleza  tunavyohusiana  na  kuwasiliana  sisi  kwa  sisi  na  wadau  pia 
·         Hufafanua  namna  tunavyofikia   maamuzi 
·         Huelezea  tunavyotumia  muda  wetu .

KUTAMBUA  USAHIHI  WA  MAADILI  HUSIKA
Ujiulize
-           Yana  hasisha  ?
-          Yameshilikishwa  /  Kila  mtu  anayafahamu  ?
-          Yanaonyesha  vipaumbele  ?
-          Yanaonesha  miongozo  ? 
-          Yanaainisha  tabia  zisizotakiwa  ?
-          Yanaendana  na  dira  na  dhamira  za  shirika?
                                   
WALENGWA
 Walengwa wa Shirika, hawa ni wahusika wanaotarajiwa kunufaika na kutokana na shughuli ambazo shirika linafanya.

4.      MUUNDO WA SHIRIKA:
Muundo wa shirika ukoje kuanzia ngazi ya juu ambayo ni uongozi mpaka ngazi ya chini yaani walengwa. Muundo uonyeshwe katika mchoro.

5.      UCHAMBUZI WA HALI/MAZINGIRA:
Uchambuzi wa Mazingira ya ndani: Hali halisi ya shirika ikoje kwa sasa. Hapa uwezo na udhaifu wa Shirika utaainishwa.
Pia uchambuzi wa mazingira ya nje ni vizuri uainishwe ili kubainisha fursa zinazoweza kusaidia shirika katika kufikia malengo yake, au vikwazo vinavyoweza kukwamisha shughuli za shirika. Uchambuzi utaangalia nyanja za kisiasa, kiuchumi, kijamii na kiteknolojia.

6.      MALENGO, SHUGHULI NA MATOKEO TARAJIWA:

MALENGO
Malengo ni hatua ambayo shirika halijafikia na hivyo linataka kufikia hatua hiyo. Yapaswa kufafanua lengo husika ambalo linataka kufikiwa. Malengo yanawekwa kwa kuzingatia vipaumbele vya shirika.
      Hapa  tunapata  lengo  kuu  na  malengo  madogomadogo   
      Huainisha  mambo  dhahiri  yatakayofikiwa .
       Malengo  huangalia  nje  zaidi  (Siyo  tunataka  kuwa)
-           Huonesha  yatavyopimwa
-          Hujibu  dhamira
      -     Kuonesha  mambo  yatakayo  sisitizwa
 Malengo  hutoa  mwongozo  wa  vipi  tutajipanga  au  tutakavyotenda kufikia  matokeo

KUTHIBITISHA  USAHIHI  WA  MALENGO
Ili kujua kama malengo ya shirika letu ni sahihi tujiulize maswali yafuatayo:
-  Yanaweza  kuonekana  ?
-  Yanapimika  ?
-  Ni dhahili  ?
-  Tumeyawekea  vipaumbele ?
-  Yanaendana  na dira  na  dhamira ya shirika letu?

SHUGHULI
Shughuli ni kazi ambazo shirika litazifanya kwa wakati husika kulingana na malengo ili kuleta matokeo tarajiwa.

MATOKEO TARAJIWA;
Ni vitu vitakavyotoa ushahidi wa mafanikio au hasira ya shughuli au mradi uliofanyika. Yanaweza kupimika kwa Idadi (yanaweza kuhesabika) au kupimika kwa kiwango cha ubora.
Kwa nini matokeo tarajiwa ni muhimu ?
n  Ni kama nyenzo  ya kuangalia mwenendo wa shughuli za shirika na pia husaidia kutambua kama matatizo.
n  Husaidia kutambua hali itakavyokuwa siku za mbeleni.
n  Yanapolinganishwa na malengo, matokeo tarajiwa huweza kuonyesha  kama hatua za kinidhamu zitahitajika kuchukuliwa na uongozi ili kurekebisha tatizo lililojitokeza, huweza kutathimini umakini wa watendaji kstika uchukuaji hatua na pia hutoa ushahidi wa namna gani malengo yamefanikiwa.

7.      MIKAKATI
Mikakati ni mbinu/njia zitakazotumika katika kutekeleza shughuli za Shirika ili kufikia malengo. Yapaswa kuelezea na kufafanua ni mikakati ipi itatumika wakati wa kutekeleza

8.      MPANGO KAZI;           
Huonyesha ni jinsi gani utekelezaji wa miradi utakavyokuwa kwa vipindi na kwa ujumla, pia huelezea rasilimali gani zitahitajika katika utekelezaji wa mradi/miradi iliyoainishwa na pia huonyesha makisio ya bajeti yatakavyo kuwa kulingana na mahitaji ya   utekelezaji wa miradi husika.
Katika mpango kazi tunajiuliza
1.      Nani atafanya nini?
2.      Nini kitafanyika lini? Na kitafanyikanye?
3.      Nini kitafanywa wapi?
4.      Vitu gani vinahitajika?
5.      Gharama zake ni kiasi gani?
6.      Matarajio ya kufanya nini ni yapi?


LENGO
SHUGHULI
ZITAKAZOFANYIKA
MUDA
RASILIMALI
GHARAMA
WALENGWA
MFUATILIAJI
MATOKEO TARAJIWA


































Chati namba 1: MPANGO KAZI





MATUMIZI
Mwaka 1
Mwaka 2
Mwaka 3
Mwaka 4
Mwaka 5
JUMLA
Shughuli za miradi






Uendeshaji wa shirika






JUMLA KUU







Chati namba 2: MAKISIO YA BAJETI



9.      UFUATILIAJI NA TATHIMINI
Kipengele hiki huelezea kwa ufupi mipango ya asasi katika kusimamia na kutathimini mwenendo wa kazi ili kuweza kupima mafanikio kwa kutoa ufafanuzi juu ya mambo yafuatayo:-
                                                                          i.            Mbinu gani zitatumka
                                                                        ii.            Dhana zitakazotumka
                                                                      iii.            Kila baada ya muda gani
                                                                      iv.            Nani watakaohusika na zoezi hilo n.k


KUMBUKA:           
                             Malengo ni ufunguo wa mafanikio &  Kupanga ni kuchagua

Yoh 3:16         Kuikomboa sayari hii ulifanyika mpango
Josh 6: 1-7       Mji wa Yeriko ulitekwa kwa mpango

 Na,
Baraka Kamese
  

Kauli mbiu yetu

BUFADESO kwa maendeleo ya wakulima

MUHIMU

Makala na picha zinazochapishwa katika blogu hii ni kwa ajili ya taarifa na kumbukumbu za Shirika la Bunda Farmers Development Support Organization (BUFADESO)
Hairuhusiwi kutumia yaliyomo katika blogu hii (HASA PICHA) kwa shughuli zozote bila ruhusa ya mmiliki wa blogu hii ambaye ni BUFADESO